Vigogo wamiminika kurejesha fomu

 IKIWA leo ndiyo siku ya mwisho kwa viongozi wa umma, kuwasilisha fomu za kuonyesha rasilimali mbalimbali walizonazo katika Ofi si za Sekretarieti ya Maadili ya Viongozi wa Umma, viongozi mbalimbali wakiwemo mawaziri, wabunge na wakuu wa wilaya ‘wamemiminika’ katika Ofi si za Sekretarieti hiyo Jijini Dar es Salaam kuwasilisha fomu hizo.
Miongoni mwa viongozi waliofika na kuwasilisha fomu zao ni Waziri wa Habari, Sanaa, Utamaduni na Michezo, Dk Harrison Mwakyembe; Mbunge wa Kigoma Kaskazini, Zitto Kabwe; Mbunge wa Kibamba, John Mnyika na Mbunge wa Ubungo, Saed Kubenea.
Wengine ni pamoja na Mkuu wa Wilaya ya Ilala, Sophia Mjema; Mkuu wa Wilaya ya Kinondoni, Ally Hapi na Mbunge wa Morogoro Kusini, Prosper Mbena. Akizungumza na waandishi wa habari, Kamishna wa Maadili, Sekretarieti ya Maadili ya Viongozi wa Umma, Jaji mstaafu Harold Nsekela alisema kumekuwepo na mwitikio mkubwa wa viongozi mbalimbali wanaofika katika ofisi hizo katika kanda zote na kuwasilisha fomu zao.
Alisema hatua hiyo imetokana na muda uliowekwa kufikia mwisho leo, hatua aliyosema kuwa kwa kiasi fulani ndiyo imesababisha kuwepo mwitikio huo mkubwa, tofauti na siku za nyuma.
“Viongozi wengi wamewasilisha fomu zao kupitia wawakilishi wao waliowatuma, kiutaratibu siyo vibaya ila wakati mwingine kunaweza kukajitokeza tatizo lolote ndani ya fomu ikizingatiwa kuwa ndani yake ina kiapo cha mhusika wa fomu,” alisema Jaji Nsekela.
Aidha alisema kutokana na mwitikio huo mkubwa, ofisi yake imeamua kufanya kazi hadi jioni siku ya jana ambayo ni nusu siku, kwa lengo la kutoa muda wa kutosha kwa viongozi mbalimbali kwenda kuwasilisha fomu zao kabla ya kufikia tamati yake hii leo.
Alisema ukiacha baadhi ya viongozi wa umma waliowasilisha fomu zao katika Jiji la Dar es Salaam, pia kupitia ofisi zake katika Kanda saba zilizopo mikoa ya Arusha, Mbeya, Tabora, Mtwara, Mwanza, Kibaha- Pwani na Dodoma, pia zimeweza kupokea fomu kutoka kwa viongozi mbalimbali hususani jana kwa ajili ya kukimbizana na muda uliobakia.
Rais John Magufuli juzi aliwasilisha fomu yake na kumwagiza Mwenyekiti wa Sekretarieti hiyo ya maadili, kusimamia muda mwisho uliowekwa na ofisi yake huku akiwaonya viongozi watakaokwepa kuwasilisha fomu hizo.
“Mheshimiwa Jaji Nsekela ikifika tarehe 31 Desemba ambayo ni siku ya mwisho kwa mujibu wa sheria, weka mstari na usipokee fomu nyingine, halafu tuone sharia itafanyaje,” alisema Rais Magufuli akimwagiza Jaji Nsekela.
Kwa upande wake, Jaji Nsekela alisema, “Viongozi hawaombwi kujaza fomu hizi, kuna baadhi wanadhani labda kutuletea hilo tamko ni fadhila, hapana, sharia ya nchi inahitaji hivyo na kuna sababu zake za msingi.”
Wakati huo huo, Waziri Mkuu Kassim Majaliwa amesema amekwishawasilisha tamko la viongozi wa umma kuhusu rasilmali na madeni kwenye Sekretarieti ya Maadili ya Viongozi wa Umma tangu juzi (Alhamisi Desemba 28, 2017).
Akizungumza na waandishi wa habari kijijini kwake Namahema ‘A’ wilayani Ruangwa mkoani Lindi jana jioni, Waziri Mkuu alisema fomu hizo zilipokelewa juzi na amekwishapatiwa barua ya kupokea tamko hilo.

Comments

Popular posts from this blog

Nyota ya Simon Msuva yazidi kungáa katika klabu yake ya Difaa El Jadid

MFANYAKAZI WA PPF AKAMATWA AKISAFIRISHA MIRUNGI

SAKATA LA AIRTEL LAZIDI KUKOLEA....TEWUTA NAO WAIBUKA