Naibu Waziri wa Viwanda, Biashara
na uwekezaji Mh. Mhandisi Stella Manyanya amefungua kikao cha siku tatu
mjini Dodoma kwa njia ya Mtandao (Video Conferece) huku akiwataka
wataalam katika ngazi ya Mikoa za Mamlaka za Serikali za Mitaa kutumia
mwanya huo kubadilishana uzoefu lakini pia kuibua fursa zilizopo katika
maeneo yao katika uanzishwaji na uendelezaji wa viwanda vidogo, vyakati
na vikubwa ifikapo 2025.
Akifungua kikao hicho Manyanya
alisema, kupitia fursa ya Viongozi hao wa Mikoa na Mamlaka za Serikali
za Mitaa kukutana kwa njia ya Mtandao kutawezesha wote kuwa na uelewa wa
pamoja kuhusu mikakati ya ujenzi wa Uchumi wa Viwanda kwakupena taarifa
za kujua viwanda vilivyopo katika maeneo yao na maendeleo yake, lakini
pia kujua maeneo yaliyotengwa mahususi kwaajili ya viwanda hivyo.
“Mkutano huu utatusaidia pia
kupambanua mikakati ya kufufua viwanda vilivyokufa na namna nzuri ya
kupata wawekezaji wapya” alisema Manyanya na kuongeza kwamba lengo la
mikutano hiyo nikuwa na mkakati endelevu yakujenga uwezo kwa watendaji
wa Mikoa na Halmashauri kuhusu masuala ya sekta ya Viwanda, Biashara na
uwekezaji.
Manyanya amesema katika awamu ya
kwanza Wakala wa Usajili Biashara na Leseni (BRELA), watatoa mafunzo juu
usajili wa Biashara, Miliki Ubunifu sambamba na ujenzi wa uchumi wa
Viwanda kama falsafa ya Mh. Rais wa awamu ya tano inavyojiapambanua
kuhusu suala zima la viwanda.
Manyanya ameongeza kuwa, Waziri wa
Nchi Ofisi ya Rais Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa Mh. Seleman
Jafo pamoja na Waziri mwenye dhamana na Viwanda, Biashara na uwekezaji
Charles Mwijage, ni viongozi ambao kwa nafasi zao wameonesha nia ya
dhati katika kuhakikisha azma iliyowekwa na Serikali ya awamu ya Tano
inatimia.
Akihitimisha risala yake ya
ufunguzi Mh. Manyanya alisema, Mikutano hiyo ni mwanzo tu, kwani
wanatarajia kuwa na chombo imara yaani kuwa na Jukwaa la Uchumi wa
Viwanda kama fursa ya kuendelea kuwezesha ujenzi na uendelezaji wa
Viwanda Nchini, ambapo wadau watajulishwa tarehe rasmi ya uzinduzi ambao
utafanywa na Mh. Waziri Mwijage.
Mkutano huo wa siku tatu kwa njia
ya mtandao ulioanza tarehe 18 na kutarajiwa kumalizika 20 Desemba, 2017
umewakutanisha Katibu Mkuu wa Wizara ya Viwanda na Biashara, Prof.
Elisante Ole Gabriel, Makatibu Tawala wa Mikoa ya Mbeya, Songwe,
Kilimnjaro, na Ruvuma, Mikoa mingine ni Kigoma, Lindi, Singida na Pwani
sambamba na wataalamu wao wa Mikoa na wale wa Halmshauri.
Comments
Post a Comment